Header Ads


BILIONI 3.7 ZATOLEWA KUKARABATI BARABARA MBEYA

MBEYA
SHILINGI Bilioni 3.7 zimetolewa na Serikali kwaajili ya ujenzi wa barabara mbalimbali jijini Mbeya kwa kiwango cha lami.
Mkuu wa mkoa wa Mbeya,Amos Makalla alibainisha hayo kwenye uzinduzi wa mradi wa ujenzi wa kipande cha barabara cha kutoka Isyesye hadi Relini jijini Mbeya chenye urefu wa kilomita 2.3.
Makalla alisema ujenzi wa kipande hicho cha barabara kitakachonufaisha kata za Isyesye na Itezi utagharimu Shilingi milioni 881.
Alisema Serikali imetenga fedha hizo kwaajili ya kuendeleza ujenzi wa barabara kwa kiwango cha lami jijini hapa na kurahisisha shughuli za usafirishaji kupitia miundombinu rafiki.
Aliwapongeza wakazi wa kata ya Isyesye waishio jirani na barabara kwa ushirikiano walioonesha kwa Serikali kwa kukubali kwa hiyari kubomoa bila fidia sehemu ya nyumba zilizokuwa ndani ya eneo linalopaswa kufikiwa na barabara.
“Mmeonesha ushirikiano mkubwa katika mradi huu.Naamini ni kwakuwa mmetambua nini Serikali inamaanisha hata ikaamua kuwajengea barabara kwa kiwacho cha lami.Maana kuna watu wengine hata kama wanapelekewa maendeleo na serikali tena kwa jambo ambalo limekuwa changamoto kwao kwa muda mrefu wao utawasikia hatutaki mpaka tulipwe fidia.Na wengine hata wakilipwa fidia bado wanakuwa wagumu.”
“Serikali inapenda watu walio na ushirikiano.Na ndiyo sababu sisi tumejipanga popote walipo wananchi wanaoonyesha ushirikiano tutapeleka miradi.Hatutaki watu wanaokaa wakati wote wanafanya siasa hao tutahamisha miradi”alisisitza Makalla.
Kwa upande wake Diwani wa kata ya Isyesye,Ibrahim Mwampwani alisema barabara ya lami ilikuwa ikisubiriwa kwa muda mrefu na wakazi wa kata za Isyesye na Itezi kutokana na adha waliyokuwa wakiipata hususani nyakati za mvua nyingi.
Alisema kujengwa kwa barabara hiyo kutakuwa kichocheo kikubwa cha maendeleo situ kwa wakazi wa kata hizo mbili bali na maeneo mengine kwakuwa watu wengi wataitumia badala ya kulazimika kupita barabara kuu pekee.

No comments

Powered by Blogger.